WAKULIMA wilayani Kahama mkoani Shinyanga wameaswa kulima mazao yanayovumilia ukame mfano zao la Arizeti katika kipindi hiki cha mabadiliko ya hali ya hewa kilimo ambacho kitakachowasaidia kujikwamua kimaisha.
Rai hiyo imetolewa leo na Lameck Sultan mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya Buzwagi Vegetable oil wakati akizungumza na waandishi wa habari ofsini kwake na kusema kuwa wakulima wengi hawanufaiki na kilimo cha mazoea wanachotumia.
Sultan amesema kipindi hiki mabadiliko ya hali ya hewa yameathiri kilimo cha mazao mbalimbali hivyo wakulima wanatakiwa kulima Arizeti ambayo matunzo yake si ya gharama kubwa.
Ameongeza kuwa katika kuhakikisha wakulima wilayani humo wananufaika na kilimo cha kisasa cha zao la Arizeti kampuni yake yake imeanza mkakati wa kuwaelimisha wakulima ili wahamasike na kilimo cha zao hilo kwa manufaa yao.
Sanjari na hayo ameiomba serikali kurekebisha mfumo wa soko la bidhaa mbalimbali zinazozalishwa nchini ihakikishe zinakuwa na soko nje ya nchi hali itakayoinua uchumi wa taifa na si kutegemea bidhaa za kigeni.
Imeelezwa kuwa wakulima wengi wa kanda ya ziwa wamejijengea desturi ya kulima mazao ya Pamba,Mpunga,tumbaku na mazao mengine ambayo kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa yamekuwa hayawanufaishi wakulima.